RAIS DKT. MAGUFULI AWASIMAMISHA TBA KUJENGA NYUMBA ZA MAGEREZA UKONGA

Описание к видео RAIS DKT. MAGUFULI AWASIMAMISHA TBA KUJENGA NYUMBA ZA MAGEREZA UKONGA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli tarehe 16 Machi, 2019 amefanya ziara ya kushtukiza katika mradi wa ujenzi wa nyumba za makazi ya Askari Magereza wa gereza la Ukonga Jijini Dar es Salaam na kuagiza mradi huo ukabidhiwe kwa Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ).
Mhe. Rais Magufuli ametoa maagizo hayo baada ya kubaini kuwa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) imeshindwa kutekeleza mradi huo kwa wakati, licha ya Serikali kutoa shilingi Bilioni 10 za ujenzi.
Ametaka wataalamu wa TBA waliokuwa wakisimamia mradi huo pamoja na Askari Magereza waondoke na kuwapisha JWTZ.
“Kwa hiyo hapa nisimuone mtu wa TBA, nisimuone mtu wa Magereza kuja kusimamia, muwaache Jeshi la Wananchi wafanye kazi zao, siku watakapokuja kunikabidhi na mimi nitawakabidhi Magereza, kwa hiyo watu wa TBA kuanzia leo nimewafukuza hapa” amesema Mhe. Rais Magufuli.
Mhe. Rais Magufuli ameelezea kutoridhishwa na utendaji kazi wa TBA katika mradio huo ambao ulianza zaidi ya miaka 2 iliyopita kwa kushirikisha Jeshi la Magereza ambalo lilikuwa linaisadia TBA katika kazi za ujenzi, na ametaka TBA na Jeshi la Magereza wabadilike katika utekelezaji wa majukumu yao.
“Nataka kila mlipo watu wa Magereza mfanye kazi, msimamie watu, kama ni ng’ombe muwafuge vizuri wazalishe vizuri hadi muuze mazao nje, kama ni kilimo mlime kwelikweli, muwe ni jeshi la kuzalisha, hii ni aibu kuleta jeshi jingine la wananchi kuja kuwajengea nyumba nyinyi, wakati nyumba mnakaa nyinyi, mlitakiwa muwe mmeshapanga mkakati kwamba TBA wamesuasua, ngoja tufyatue matofari, tuanze kujenga” amesisitiza Mhe. Rais Magufuli.
Mkuu wa Utawala wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) Kanali Charles Mbuge amesema JKT itakamilisha ujenzi huo ndani ya kipindi cha miezi 2 na nusu kuanzia kesho na kwamba kazi zitafanywa usiku na mchana.
Aidha, Mhe. Rais Magufuli ameitaka TBA kutoa maelezo ya namna fedha zilizotolewa na Serikali kiasi cha shilingi Bilioni 10 zilivyotumika, na ameonya kuwa endapo itabainika matumizi ya fedha hizo hayaendani na kazi zilizofanyika hatua kali zitachukuliwa.
Katika mradi huo, ujenzi wa majengo 12 ya makazi ya Askari Magereza yaliyopangwa kuwa na ghorofa 4 kila moja ulioanza Desemba 2016 umefikia asilimia 45 tu na unaendelea kwa kusuasua.

Комментарии

Информация по комментариям в разработке