HOTUBA YA RAIS DKT JOHN POMBE MAGUFULI AFUNGUA UWANJA WA NDEGE WA BUKOBA

Описание к видео HOTUBA YA RAIS DKT JOHN POMBE MAGUFULI AFUNGUA UWANJA WA NDEGE WA BUKOBA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amefungua miundombinu mipya ya uwanja wa ndege wa Bukoba Mkoani Kagera na kuiagiza Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kuachana na mpango wa kujenga uwanja mpya katika eneo la Omukajunguti na badala yake waongeze urefu wa barabara ya kurukia ndege katika uwanja wa ndege wa Bukoba ili ndege kubwa zaidi ziweze kutumia uwanja huo.
Mhe. Rais Magufuli aliyeongozana na Mkewe Mama Janeth Magufuli amesema ujenzi wa uwanja mpya katika eneo la Omukajunguti utasababisha Serikali kutumia fedha nyingi bila sababu zikiwemo Shilingi Bilioni 9.2 za kulipa fidia na gharama kubwa za kujenga uwanja katika eneo hilo chepechepe.
Hata hivyo Mhe. Dkt. Magufuli ameipongeza Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA), Wakandarasi Wazalendo waliojenga uwanja wa ndege Bukoba na wananchi wa Bukoba kwa kufanikisha ujenzi wa uwanja huo ambao utasaidia kuchochea uchumi kwa kuendeleza na kukuza utalii, ujenzi wa viwanda na biashara mbalimbali.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TAA Bw. Richard Mayongela amemueleza Mhe. Rais Magufuli kuwa kazi za ujenzi, upanuzi na ukarabati wa uwanja huo zimehusisha ujenzi wa barabara ya kurukia ndege yenye urefu wa mita 1,500 na upana wa mita 30, ujenzi wa eneo la kuegesha ndege, ujenzi wa eneo la kuegesha magari, ujenzi wa jengo la abiria, kituo cha kuzalisha umeme wa dharula na kufunga mifumo ya kisasa ya ukaguzi, ubebaji mizigo na kurekodi matukio (CCTV).
Bw. Mayongela amesema ujenzi, upanuzi na ukarabati huo umegharimu Shilingi Bilioni 31.95 ambapo kati yake Shilingi Bilioni 6.35 zimetolewa na Serikali ya Tanzania na fedha nyingine zimetolewa kwa mkopo nafuu kutoka Benki ya Dunia.
Nae Mwakilishi wa Benki ya Dunia Bw. Andre Bald amempongeza Mhe. Rais Magufuli kwa Tanzania kuwa na uchumi unaokuwa vizuri na kwa kasi na ameelezea kufurahishwa na matunda ya ushirikiano kati ya Tanzania na Benki ya Dunia katika kufanikisha miradi mbalimbali nchini ukiwemo mradi wa uwanja wa ndege wa Bukoba.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa Mnyaa amesema mradi wa ujenzi, upanuzi na ukarabati wa uwanja wa ndege wa Bukoba ni moja ya miradi mitatu inayotekelezwa, mingine ikiwa ni viwanja vya ndege vya Tabora na Kigoma ambapo Benki ya Dunia imetoa mkopo nafuu wa Shilingi Bilioni 129 na Serikali ya Tanzania imetoa Shilingi Bilioni 26.
Prof. Mbarawa ameongeza kuwa katika mwaka huu wa fedha Serikali itafanya upembuzi yakinifu katika viwanja vya ndege 11 hapa nchini ambavyo ni Singida, Lindi, Njombe, Iringa, Musoma, Ziwa Manyara, Kilwa Masoko, Songea, Tanga, Moshi na Simiyu na kwamba kati ya viwanja hivyo upanuzi na ukarabati utafanyika katika viwanja vya ndege vya Songea, Iringa na Musoma katika mwaka huu wa fedha.
Wakati huo huo, Mhe. Rais Magufuli amesema Serikali itaanza kulipa stahili mbalimbali za wafanyakazi kuanzia mwezi huu na kubainisha kuwa malipo hayo yanafanyika baada ya kufanya uhakiki ambao umesaidia kutambua udanganyifu mkubwa katika baadhi ya madai ya wafanyakazi.
Ametoa mfano wa baadhi ya wadai hao kuwa ni Jakson Kaswahili Robert wa Ukerewe anayedai Shilingi Bilioni 7 na Milioni 626 wakati uhakiki umebaini kuwa hadai kitu, Mwachano Ramadhan Msingwa wa Bagamoyo anayedai Shilingi Bilioni 1 na Milioni 754 wakati uhakiki umebaini kuwa anadai Shilingi Milioni 2 na Gideon Zakayo anayedai Milioni 104, na ameagiza vyombo vya dola kuwachunguza wafanyakazi hao pamoja na watumishi wa Menejimenti ya Utumishi wa Umma ambao waliidhinishi watu hao walipwe madai hayo.
Mhe. Rais Magufuli amesema katika jitihada za kuwajali wafanyakazi Serikali imetoa Shilingi Trilioni 1.2 kulipa madeni ya mifuko ya hifadhi ya jamii na ameeleza kuwa ili kuongeza ufanisi Serikali inapeleka bungeni muswada wa kuunganisha mifuko ya hifadhi ya jamii ili ibaki mifuko miwili, mmoja utakaoshughulikia wafanyakazi wa umma na mwingine utakaoshughulikia wateja kutoka sekta binafsi.
Ametoa wito kwa Watanzania kuendelea kuunga mkono juhudi mbalimbali za Serikali ya Awamu ya Tano na amewataka wanasomi wakiwemo wanasheria kusaidia kupigania maslahi ya nchi ikiwemo kesi mbalimbali zilizofunguliwa katika mahakama za kimataifa na juhudi za kupigania rasilimali za Taifa badala ya kupinga mitandaoni.
Sherehe hizo zimehudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge inayoshughulikia miundombinu, Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani, Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Mhe. Charles Mwijage na Wabunge wa Mkoa wa Kagera.

Комментарии

Информация по комментариям в разработке