Katika video hii inazungumza kuhusu sababu, dalili, matibabu, namna ya kuzuia, matarajio baada ya matibabu ya KIUNGULIA , endelea angalia mpaka mwisho kujifunza.
Kiungulia (heartburn) ni hali ya kuhisi mchomo (maumivu kama moto) unaotokea nyuma ya mfupa wa kidari. Kwa kawaida maumivu haya yanaanzia kwenye umio (oesophagus) na kupanda kifuani na yanaweza kuenea mpaka kwenye shingo au koo.
Karibu kila mtu anapatwa na kiungulia kwa wakati fulani katika maisha yake. Kama unapata kiungulia mara kwa mara, unaweza kuwa na ugonjwa unaosababishwa na kucheua mara kwa mara unaoitwa gastroesophageal reflux disease.
Katika hali ya kawaida, chakula kinapoingia tumboni, ukanda wa misuli ulio mwishoni mwa umio unakaza na kukifungia chakula tumboni. Ukanda huu unaoitwa lower esophageal sphincter unafanya kazi muhimu ya kuzuia chakula cha tumboni kurudi juu.
Kama huu ukanda hautafunga vizuri au utalegea, asidi zinazosaidia kumeng’enya chakula zilizo tumboni, zinaweza kurudi juu kwenye umio na kusababisha hisia ya mchomo - kiungulia
Nani yuko katika hatari zaidi ya kupata kiungulia?
Ujauzito na dawa mbalimbali zinaweza kusababisha kiungulia.
Kwa wanawake wajawazito - kiungulia kinatokea kwa sababu mtoto anakua na kusukuma tumbo juu zaidi kuliko kawaida. Kwa sababu tumbo linabanwa na mtoto - asidi zilizo tumboni zinasukumwa kwenda juu kwenye umio na kusababisha mchomo. Tatizo la kiungulia linaisha kabisa baada ya mjamzito kujifungua.
Zipi dawa mbalimbali ukizitumia zinaweza kusababisha kiungulia – madawa kama ya kuzuia kutapika, dawa za presha au ugonjwa wa moyo, dawa za uzazi wa mpango, dawa za usingizi, na baadhi ya dawa za pumu.
Kama unafikiri moja ya dawa zako inasababisha kiungulia , ongea na daktari. USIBADILI au KUACHA kutumia dawa bila kuzungumza na daktari.
Wakati gani utafute matibabu ya haraka?
Kwa sababu kiungulia ni tatizo linalowapata watu wengi, nadhani ni vizuri kujua ni wakati gani unapopaswa kwenda kupata matibabu.
Unapaswa kupata matibabu haraka sana kama una kiungulia na:
• Unatapika matapishi yenye damu au yanayoonekana kama kahawa
• Kinyesi chako ni cheusi (kama lami) au cha rangi ya damu ya mzee
Mwone daktari kama:
• Unapata kiungulia mara kwa mara
• Unapungua uzito bila sababu maalumu
• Unapata shida kumeza (unahisi kama chakula kinakwama kooni)
• Una kikohozi au mkoroto (wheeze) usioisha
• Kiungulia kinazidi zaidi baada ya kutumia dawa za kupunguza asidi tumboni
Utambuzi wa kiungulia
Kwa kawaida, kutambua kiungulia ni rahisi sana kutokana na dalili utakazomweleza daktari. Daktari atafanya uchunguzi wa mwili na kuuliza maswali kadhaa kuhusu tatizo lako – anaweza pia kuagiza kipimo kinachotumia kamera ndogo inayoingizwa kupitia mdomoni kukagua umio, tumbo na utumbo kama itahitajika – Esophagogastroduodenoscopy
Uchaguzi wa matibabu ya kiungulia
Unapaswa kutibiwa kiunguli hasa kama kinatokea mara kwa mara. Kama kiungulia kitakuwepo kwa muda mrefu, asidi zinaweza kuharibu utando ute wa ndani ya umio na kusababisha matatizo makubwa.
Habari njema, ni kuwa ukibadilisha tabia na mfumo wa maisha unaweza kuzuia kiungulia au kupunguza dalili.
Vidokezo vifuatavyo vinaweza kusaidia kuzuia kingulia. Kama hatua hizi hazitafanikiwa kupunguza dalili zako, mwone daktari.
Kwanza, jaribu kuepuka vyakula na vinywaji vinaweza kusababisha ucheue, kama vile:
• Pombe
• Kahawa/energy drinks
• Vinywaji vyenye kaboni-mf; soda
• Chokoleti
• Matunda na juisi za jamii ya mchungwa,mlimau, mdimu n.k
• Vyakula vyenye viungo vingi, mafuta, na bidhaa za maziwa
• Nyanya na sosi za nyanya
Kisha, jaribu kubadili tabia ya ulaji wako:
• Epuka kuinama au kufanya mazoezi baada tu ya kula.
• Epuka kulala masaa 3 - 4 baada ya kula. Kulala tumbo likiwa limejaa husababisha chakula kusukuma kwa nguvu ukanda unaozuia chakula
• Kula chakula kidogo.
Fanya mabadiliko mengine katika maisha yako kama inavyohitajika:
• Epuka kuvaa mikanda au nguo zinazobana sana kiuno na tumbo – mikanda inaweza kubana tumbo na kusababisha chakula kupanda juu.
• Punguza uzito kama wewe ni mnene. Kitambi kinaongeza shinikizo ndani ya tumbo.
• Lala kichwa kikiwa kimenyanyuliwa kwa angalau kwa sentimeta 3 hivi. Kulala kichwa kikiwa juu kidogo kuliko tumbo kunasaidia kuzuia chakula kilichomeng’enywa kurudi nyuma. Weka vitabu, tofali au mito chini ya godoro kwenye maeneo ya kichwa. Kulalia mito mingi haisaidii kupunguza kiungulia kwa sababu unaweza kuteleza na kutoka kwenye mto usiku. Weka mito chini ya godoro ili kulinyanyua.
• Acha kuvuta sigara, kemikali katika moshi wa sigara hulegeza ukanda unaofunga sehemu ya chini ya umio.
Kama bado haujapata nafuu vizuri, jaribu kutumia dawa.
• Dawa za kupunguza asidi tumboni (Antacids), zinasawazisha asidi iliyo tumbo. Zipo dawa aina nyingi – nenda kwenye duka la dawa utazipata.
Emmanuel Mniko #mniko #wikielimu @wikielimu
Информация по комментариям в разработке