Katika video hii inazungumza kuhusu sababu, dalili, matibabu, namna ya kuzuia, matarajio baada ya matibabu ya VVU/UKIMWI, endelea angalia mpaka mwisho kujifunza
Ugonjwa mbaya unaotishia maisha uliotambuliwa mara ya kwanza Tanzania mkoani Kagera mwaka 1983. Ugonjwa wa UKIMWI inatokana na kuwa na maambukizi ya muda mrefu ya virusi vya ukimwi (VVU), ambao mara nyingi kadri muda unavyoenda yanasababisha uharibifu wa mfumo wa kinga ya mwili na viungo vya mwili, pamoja mfumo wa fahamu. Ugonjwa huu ni janga la dunia nzima.
Tuna aina mbili za virusi vya ukimwi (VVU), aina ya 1 na ya 2.
VVU-1 ni maambukzi yaliyosambaa dunia nzima, lakini yanapatikana zaidi Kusini mwa jangwa la sahara, Amerika, Kusini mwa ulaya na kusini-mashariki mwa bara Asia. VVU-2 inapatikana zaidi Afrika magharibi.
Ripoti ya wizara ya afya 2022 -2023 ya Tanzania inasema:
• Kiwango cha maambukizi ya VVU kama nchi kwa ujumla inakadiriwa kuwa ni 4.4 % - hii ni sawa na watu 1,548,000 wanaoishi na maambukizi
• Kiwango cha maambukizi mapya 60,000 kila mwaka (15 -49)
• Kiwango cha maambukizi mapya kwa watoto chini miaka 15 ni 6,500
• Karibia 50% ya maambukizi yote mapya yanawapata vijana umri wa 15-29
Takwimu hizi zinaogopesha kwa sababu kati ya magonjwa 10 yanayosababisha ulemavu na vifo vingi nchini, UKIMWI ni ya nne.
Uambukizo
Unaweza kuambukizwa Virusi vya ukimwi kwa;
• Kujamiana na mtu mwenye maambukizi bila kinga
• Kushika majimaji au damu ya mtu maambukizi – hasa kwa kuchangia vitu vyenye ncha kali kama wembe au sindano
• Kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto
Ukishaambukizwa, haifahamiki vyema ni baada ya muda gani unaweza kuambukiza wengine – lakini baadhi ya wataalamu wanadhani kwamba unaweza kumwambukiza mwingine muda mfupi tu baada ya kuambukizwa.
Nani yuko kwenye hatari
Watu wote wako kwenye hatari. Hatari ya kuambukizwa inaongezeka zaidi kama una magonjwa mengine ya ngono, hasa yanayosababisha vidonda.
Dalili
Muda wa dalili kuanza baada ya kuambukizwa inatofautia kwa kila mtu. Kwa watu wengi dalili zinaanza kuonekana mwaka 1 mpaka mwaka 10 au zaidi baada ya kuambukizwa. Karibia nusu ya watu wote wenye maambukizi watakuwa wameanza kuonesha dalili (UKIMWI) ndani ya miaka 10.
Dalili za ugonjwa wa UKIMWI zimegawanyika katika makundi mawili
1. Dalili za awali
o Zinatokea wiki 3-6 baada ya maambukizi
o Dalili hizi ni: homa, vidonda mdomoni, ukeni au ndani ya pua, maumivu ya koo, kuvimba mtoki, maumivu ya kichwa, maumivu nyuma ya jicho, maumivu ya viungo, maumivu ya misuli, uchovu, kichefuchefu, , kutapika na kuhara
o Dalili zote hizo – huwa zinapona zenyewe baada ya muda.
• Baada ya dalili hizo za awali, mgonjwa anaweza kuishi kwa muda mrefu bila kuwa na dalili kubwa – hasa kama anatumia dawa za kufubaza VVU – anaweza kuishi mwaka 1 – 10 bila kuwa na dalili zozote. Baadae anaanza tena kupata dalili
2. Dalili zinazotokea baadae
o Hizi zinatokea kwa sababu ya magonjwa nyemelezi kama zile nimonia inayosababishwa na fangasi, Kifua kikuu, kuvimba kwa utando unaofunika ubongo na uti wa mgongo (hasa husababishwa na fangasi cryptococcal) na magonjwa mengine nyemelezi
• Katika kipindi hiki, hali ya mgonjwa inaweza kudhoofu haraka sana na hata kusababisha kifo kama hatapatiwa matibabu sahihi
Utambuzi
• Kwa vipimo vilivyopo kwenye hospitali zetu, unaweza kutambuliwa kwamba ina ugonjwa wa ukimwi miezi 3 baada ya kuambukizwa. Na ndio maana, ukienda kupima ukapatikana hauna maambukizi – madktari wanakwambia urudi tena baada ya miezi mitatu ili urudie kupima tena.
• Angalizo ni kwamba, dalili nyingi za ugonjwa wa ukimwi zinafanana na zile zinazosababishwa na magonjwa mengine – kwa hiyo, hauwezi kusema mtu ameambukizwa VVU kwa kuangalia dalili pekee. Unahitaji kufanyiwa vipimo ili kuhakikisha
• Kama una wasiwasi, nenda kituo cha afya ufanyiwe uchunguzi.
Dr. Emmanuel Mniko #mniko #wikielimu @wikielimu
Информация по комментариям в разработке